MTUKUZE MUNGU, SI MWANADAMU
KATIKA miezi ya hivi karibuni,
watu wanaopenda uadilifu duniani walijifunza jinsi ya kumtukuza Mungu
kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya “Mtukuzeni
Mungu.” Na tupitie programu yenye kuelimisha ya kusanyiko hilo.
Kwa wahudhuriaji walio wengi
programu hiyo iliyotegemea Biblia iliendelea kwa siku tatu mfululizo,
lakini kwa wale waliohudhuria makusanyiko ya pekee ya kimataifa,
programu hiyo ilichukua siku nne. Kwa ujumla, wahudhuriaji walisikiliza
hotuba za Kimaandiko zaidi ya 30, na baadhi ya hotuba hizo ziliwasaidia
wathamini zaidi mambo ya kiroho. Mambo yaliyoonwa yaliwaimarisha imani,
maonyesho yakakazia jinsi ya kutumia kanuni za Biblia, nayo drama
iliyoigizwa kwa mavazi maalumu ikaonyesha magumu ambayo Wakristo wa
karne ya kwanza walikabili. Ikiwa ulihudhuria mojawapo ya makusanyiko
hayo, kwa nini usipitie maandishi yako unaposoma makala hii? Tuna hakika
kwamba ukifanya hivyo utakumbuka mambo mengi mazuri ya kiroho ambayo
pia ni yenye kuelimisha.
Kichwa cha Siku ya Kwanza: “Wewe Wastahili, Yehova, . . . Kupokea Utukufu”
Baada ya wimbo na sala ya
kufungua, msemaji wa kwanza aliwakaribisha wote kwa uchangamfu kupitia
hotuba iliyokazia sababu kuu ya kusanyiko hilo: “Tumekusanyika ili
Kumtukuza Mungu.” Akinukuu Ufunuo 4:11,
msemaji alikazia kichwa kikuu cha kusanyiko. Baada ya hapo alifafanua
maana ya kumtukuza Mungu. Akitumia kitabu cha Zaburi, alikazia kwamba
kumtukuza Mungu kunatia ndani “ibada,” ‘utoaji shukrani,’ na “sifa.”—Zaburi 95:6; 100:4, 5; 111:1, 2.
Hotuba iliyofuata ilikuwa na
kichwa “Wanaomtukuza Mungu Hubarikiwa.” Msemaji alitaja jambo fulani
lenye kupendeza. Kwa kuwa kuna Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita
katika nchi 234 duniani, tunaweza kusema kwamba wanamtukuza Yehova
mchana na usiku. (Ufunuo 7:15) Wasikilizaji walitiwa moyo wakati ndugu na dada kadhaa Wakristo walio katika aina fulani ya utumishi wa pekee walipohojiwa.
Hotuba iliyofuata ilikuwa na
kichwa “Uumbaji Unatangaza Utukufu wa Mungu.” Ingawa mbingu halisi
hazisemi chochote, zinautukuza ukuu wa Mungu na kutusaidia tuthamini
zaidi utunzaji wake wenye upendo. Jambo hilo lilifafanuliwa kwa undani
zaidi.—Isaya 40:26.
Mateso, upinzani, uvutano wa
ulimwengu, na maelekeo yenye dhambi hujaribu uaminifu wa maadili wa
Wakristo wa kweli. Hivyo, wasikilizaji walihitaji kusikiliza kwa makini
hotuba yenye kichwa “Tembea kwa Uaminifu wa Maadili.” Msemaji
alizungumzia Zaburi ya 26 mstari kwa mstari na kuwahoji wanashule wawili
Mashahidi. Mmoja wao alidumisha msimamo imara wa maadili na yule
mwingine alikuwa akitumia wakati mwingi kwenye vitumbuizo visivyofaa
lakini akachukua hatua kushinda tatizo hilo.
Kichwa cha hotuba ya msingi
kilikuwa, “Maono Matukufu ya Kinabii Hutuchochea!” Msemaji alitaja
vielelezo vya nabii Danieli na mitume Yohana na Petro kuwa watu ambao
imani yao ilitiwa nguvu na maono matukufu ya kinabii yaliyohusu
kusimamishwa na kuanza kufanya kazi kwa Ufalme wa Mungu wa Kimasihi.
Msemaji alisema hivi kuhusu mtu yeyote ambaye huenda amesahau
uthibitisho ulio wazi kwamba tunaishi wakati wa mwisho: “Tunatumaini kwa
unyofu kwamba watu hao watakaza tena macho yao kwenye uhalisi wa kuwapo
kwa Kristo katika utukufu wa Ufalme nao watasaidiwa wapate tena nguvu
za kiroho.” Programu ya asubuhi kwenye makusanyiko ya Kiswahili
imalizika kwa hotuba yenye kichwa, “Hatua Muhimu ya Kiroho!” ambapo
Biblia nzima ya New World Translation ilitolewa katika Kiswahili.
Programu ya alasiri ilianza kwa
hotuba yenye kichwa “Yehova Huwafunulia Wanyenyekevu Utukufu Wake.”
Msemaji alionyesha jinsi Yehova anavyoweka kielelezo cha unyenyekevu,
ingawa yeye ndiye Mkuu zaidi katika ulimwengu wote. (Zaburi 18:35)
Wale walio wanyenyekevu kikweli hupata kibali cha Yehova, lakini yeye
huwapinga wale ambao hujifanya kuwa wanyenyekevu wanaposhughulika na
watu wa umri wao au wakubwa wao huku wakiwatendea kwa ukali wale walio
chini ya uongozi wao.—Zaburi 138:6.
Halafu, unabii wa Biblia
ukazungumziwa katika mfululizo wa hotuba zilizokazia mambo mbalimbali
kuhusu kichwa kikuu: “Unabii wa Amosi—Ujumbe Wake kwa Ajili ya Siku
Zetu.” Msemaji wa kwanza alitaja kielelezo cha Amosi na kuonyesha daraka
letu la kuwaonya watu kuhusu hukumu ya Yehova inayokuja. Kichwa cha
hotuba yake kilikuwa “Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri.” Msemaji wa pili
aliuliza hivi: “Je, Yehova atakuja kukomesha uovu na mateso katika dunia
hii?” Hotuba yake yenye kichwa, “Hukumu ya Mungu Juu ya Waovu,”
ilionyesha kwamba sikuzote hukumu ya Mungu ni ya haki, haiepukiki, nayo
huchagua. Msemaji wa mwisho katika mfululizo huo alikazia kichwa “Yehova
Huuchunguza Moyo.” Wale wanaotamani kumpendeza Yehova watatii maneno
haya ya Amosi 5:15: “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.”
Vileo, kama vile divai ambayo
hufurahisha moyo, vinaweza kutumiwa vibaya. Katika hotuba yake “Epuka
Mtego wa Kutumia Kileo Kupita Kiasi,” msemaji alitaja hatari za kimwili
na za kiroho za kutumia kileo kupita kiasi, hata kama mtu hatalewa.
Alitaja kanuni inayotoa mwongozo: Kwa kuwa watu wana uwezo mbalimbali wa
kustahimili kileo, kiasi chochote cha kileo kinachokufanya usiwe na
“hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri” kimepita kiasi.—Methali 3:21, 22.
Kwa kuwa tunaishi katika nyakati
za hatari, hotuba iliyofuata, “Yehova, ‘Ngome Yetu Wakati wa Taabu,’”
ilikuwa yenye kufariji. Sala, roho takatifu, na Wakristo wenzetu
wanaweza kutusaidia kuvumilia.
Hotuba ya mwisho siku hiyo,
“Nchi Nzuri—Mwonjo wa Paradiso,” ilimalizika kwa jambo lililowasisimua
na kuwafurahisha wote, yaani, kutolewa kwa kichapo kipya chenye ramani
nyingi za Biblia! Kina kichwa.
Kichwa cha Siku ya Pili: “Wahubirini Mataifa Habari za Utukufu Wake”
Baada ya kuchunguza andiko la
siku, mfululizo wa pili kwenye kusanyiko ulitolewa nao ulikuwa na
kichwa, ‘Tutoe Kama Vioo Mrudisho wa Utukufu wa Yehova.’ Hotuba ya
kwanza ilizungumzia jinsi tunavyoweza ‘Kueneza Habari Njema Kila Mahali’
nayo ilitia ndani maigizo ya mambo halisi yaliyoonwa katika utumishi wa
shambani. Katika hotuba ya pili iliyokuwa na onyesho kuhusu ziara ya
kurudia, msemaji alizungumzia kichwa, “Kuondoa Shela Kutoka kwa Wale
Waliopofushwa.” Mahojiano yenye kuvutia kuhusu mambo yaliyoonwa katika
utumishi yalifanya hotuba ya mwisho ya mfululizo huo ambayo ilikuwa na
kichwa “Tufanye Hivyo kwa Ukamili Zaidi Katika Huduma Yetu,” iwe yenye
kupendeza.
Hotuba iliyofuata kwenye
programu ilikuwa na kichwa “Wanachukiwa Bila Sababu.” Ilikuwa na
mahojiano yenye kutia moyo ya watu waaminifu ambao kwa nguvu za Mungu
walidumisha uaminifu-maadili chini ya upinzani.
Baada ya hotuba ya ubatizo ambayo hungojewa kwa hamu sana, wote wanaostahili
hubatizwa kwa kuzamishwa kabisa katika maji. Ubatizo wa maji huonyesha
kwamba mtu amejiweka wakfu kabisa kwa Yehova. Hivyo, kichwa cha hotuba
hiyo kilifaa sana: “Kuishi Kulingana na Wakfu Wetu Humtukuza Mungu.”
Programu ya alasiri ilianza kwa
hotuba iliyowatia moyo wasikilizaji wajichunguze, “Kusitawisha Maoni ya
Kristo Kuhusu Umashuhuri.” Msemaji alitaja jambo hili lenye kupendeza:
Tunapata umashuhuri kwa kuiga unyenyekevu wa Kristo. Hivyo, Mkristo
hapaswi kutafuta madaraka ili kutosheleza tamaa ya kibinafsi. Anapaswa
kujiuliza, ‘Je, mimi niko tayari kufanya kazi zenye kusaidia wengine
ambazo hazitatambuliwa kwa urahisi?’
Je, wewe huchoka? Jibu ni wazi.
Wote walifurahia hotuba “Kuchoka Kimwili Wala Si Kiroho.” Mahojiano na
Mashahidi waliotumikia kwa muda mrefu yalionyesha kwamba Yehova anaweza
kutufanya ‘tuwe na uwezo kupitia roho yake.’—Waefeso 3:16.
Tunaweza kujizoeza sifa ya
ukarimu ingawa hatuzaliwi nayo. Jambo hilo muhimu lilikaziwa katika
hotuba “Tuwe Wakarimu, Tayari Kushiriki.” Kisha swali hili lenye kuamsha
fikira likaulizwa: “Je, sisi tuko tayari kutumia dakika kadhaa kwa siku
tukiwa pamoja na ndugu na dada walio wazee, wagonjwa, walioshuka moyo,
au walio wapweke?”
Wasikilizaji walivutiwa na
hotuba “Jihadhari na ‘Sauti ya Wageni.’” Hotuba hii iliwalinganisha
wafuasi wa Yesu na kondoo ambao husikiliza sauti yake tu akiwa
“mchungaji mwema” na ambao hawaisikilizi “sauti ya wageni” inayotokana
na vyanzo vingi vya kibinadamu vyenye uvutano wa Ibilisi.—Yohana 10:5, 14, 27.
Lazima waimbaji wa kwaya waimbe
kwa upatano ili waeleweke. Ili kumtukuza Mungu, ni lazima waabudu wa
kweli duniani pote wawe na umoja. Hivyo, hotuba “Kumtukuza Mungu ‘kwa
Kinywa Kimoja’” ilitoa maagizo yenye manufaa kuhusu jinsi sote
tunavyoweza kusema “lugha safi” na kumtumikia Yehova “bega kwa bega.”—Sefania 3:9.
Wazazi, hasa wale walio na
watoto wadogo walifurahia sana hotuba ya mwisho ya siku hiyo, “Watoto
Wetu Ni Urithi Wenye Thamani.” Wasikilizaji walifurahi na kushangaa
wakati kitabu kipya chenye kurasa 256 kilipotolewa. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kitawasaidia wazazi watumie wakati kwa njia yenye kunufaisha kiroho pamoja na watoto ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu.
ENDELEA KUFUATILIA MFULULIZO WA NENO LA MUNGU KILA SIKU KUPITIA BLOG HII NA THE BLOGER, MGALULA Y.J.
Kichwa cha Siku ya Tatu: “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”
Siku ya mwisho ya kusanyiko
ilianza kwa wazo la kiroho kupitia vikumbusho vya andiko la siku. Sehemu
ya kwanza ya programu ya siku hiyo ilikazia fikira zaidi familia.
Hotuba ya kwanza, “Enyi Wazazi, Jengeni Familia Zenu,” iliwatayarisha
wasikilizaji. Baada ya kuzungumzia madaraka ya wazazi ya kuandaa
mahitaji ya kimwili ya familia zao, msemaji alithibitisha kwamba daraka
kuu la wazazi ni kuwaandalia watoto wao mahitaji ya kiroho.
Msemaji aliyefuata alizungumza
kuhusu watoto katika hotuba yenye kichwa “Jinsi Vijana Wanavyomsifu
Yehova.” Alisema kwamba vijana ni kama “matone ya umande” kwa sababu ni
wengi na nguvu yao ya ujana huburudisha. Watu wazima hufurahi kumtumikia
Yehova pamoja na vijana. (Zaburi 110:3) Hotuba hiyo ilikuwa na mahojiano yenye kuvutia ya vijana wenye mfano mzuri.
Sikuzote drama za Biblia ambazo
huigizwa kwa mavazi maalumu, ni sehemu yenye kuvutia ya makusanyiko ya
wilaya. Kusanyiko hilo lilikuwa na drama kama hiyo. Drama yenye kichwa
“Kuhubiri kwa Ujasiri Licha ya Upinzani” iliigiza wafuasi wa Yesu wa
karne ya kwanza. Drama hiyo ilikuwa yenye kufurahisha, na hasa yenye
kufundisha. Hotuba iliyofuata drama hiyo, “Tangaza Habari Njema ‘Bila
Kuacha,’” ilikazia mambo makuu ya drama hiyo.
Wahudhuriaji wote walitazamia
kwa hamu jambo kuu katika programu ya Jumapili, yaani hotuba ya watu
wote “Ni Nani Wanaomtukuza Mungu Leo?” Msemaji alithibitisha jinsi
wanasayansi na wanadini kwa ujumla hawamtukuzi Mungu. Watu wanaoitwa kwa
jina lake tu, ambao wanahubiri na kufundisha kweli kumhusu Yehova, ndio
wanaotukuza kikweli jina lake leo.
Hotuba ya watu wote ilifuatwa na muhtasari wa funzo la Mnara wa Mlinzi
la juma hilo. Kisha ikafuata hotuba ya mwisho, “‘Endeleeni Kuzaa
Matunda Mengi’ ili Kumtukuza Yehova.” Msemaji aliwasomea wasikilizaji
azimio lenye mambo kumi yaliyokazia njia mbalimbali za kumtukuza Yehova,
Muumba, na kuwaomba walikubali. Wote katika makusanyiko yote duniani
waliitikia kwa kusema “Ndiyo.”
Hivyo, kusanyiko lilipomalizika
kila mtu aliyehudhuria alikuwa akikumbuka kichwa “Mtukuzeni Mungu.”
Sikuzote na tujitahidi kumtukuza Mungu wala si wanadamu kwa msaada wa
roho ya Yehova na tengenezo lake linaloonekana.