Tuesday, 30 April 2013

WANAUME MBEYA WAJITOKEZA KWA WINGI KUPIMA KISUKARI NA SHINIKIZO LA DAMU KUFUATIA BIMA YA AFYA KUPIMA BURE UWANJA WA SOKOINE IKIWA NI MAADHIMISHO YA MEI MOSI INAYOFANYIKA KITAIFA MKOANI MBEYA HUKU WANAWAKE WAKITAKA KUPIMA UKIMWI


BAADHI YA MAAFISA WA MFUKO WA BIMA YA AFYA MKOANI MBEYA WAKIWA KWENYE BANDA LA UPIMAJI WA AFYA BURE, HUDUMA INAYOTOLEWA NA MFUKO HUO AMBAPO BAADA YA KUPIMWA WANANCHI HUPEWA USHAURI.

Na Mgalula Joseph, Mbeya
WANAUME mkoani Mbeya wengi wamejitokeza kupima magonjwa ya Kisukari na shinikizo la damu huku wanawake wakijitokeza kwa wingi kupima VVU.
Hali hiyo imebainika katika banda la mfuko wa taifa wa bima ya afya(NHIF)lililopo katika uwanja wa Sokoine ambako mfuko huo unatoa huduma ya upimaji bure ikiwa ni kuazimisha siku kuu ya wafanya kazi (Mei mosi) inayofanyika kitaifa mkoani hapa na mgeni rasmi ni Rais Jakaya Kikwete.
Akizungumza na Mtandao wa www.kalulunga.blogspot.com afisa uhakiki na ubora wa mfuko huo, Dr. Lucas Gama, alisema kuwa wananchi wengi wameendelea kujitokeza kupima afya zao tangu jana wakiwemo wanawake na wanaume hasa vijana.
‘’Wanajitokeza kwa wingi, lakini wanawake wengi wanaokuja wanasema wanataka kupima Ukimwi wakati wanaume wanaokuja wanauliza tunapima nini na tukiwaambia tunapima Kisukari na shinikizo la damu wanaongezeka kuja kupima’’ anasema Dr. Gama.
Alisema kuwa imejengeka tabia kwa baadhi ya wananchi kuona kuwa Ukimwi ni ugonjwa hatara wakati ugonjwa huo hauuwi haraka tofauti na magonjwa kama kisukari na shinikizo la damu(BP).
‘’Magonjwa haya ni magonjwa hatari na yanaua haraka kuliko Ukimwi, jana tumewapata wagonjwa watatu ambao wana sukari 200 jambo ambalo ni hatari sana na tumewapa ushauri na hapo utagundua kuwa watu wanatembea na majeneza’’ alisema Dr. Gama.
Alifafanua kuhusu magonjwa hayo kuwa shirika la afya duniani(WHO), linasema kuwa Sukari na shinikizo la damu ni viashiria vya afya ya mtu, ambapo sukari ikiwa 7 kwenda chini ni sukari ya kawaida ila kwenda juu mtu akiwa hajala ni hatari.
Kwa upande wake afisa wa NHIF mkoa wa Mbeya Reginald Kileo, alisema kuwa mfuko huo umeona umuhimu wa kutoa huduma hiyo bure ili  wananchi waweze kuwa na mazoea ya kupima afya zao.
‘’Watu wanatembea na makaburi lakini hawajui, hivyo ni muhimu serikali ikaendelea kutoa elimu kwa wananchi kujitokeza kupima afya zao na iwe bure’’ alisema Kileo.
Mwananchi Agness Mojo mkazi wa Soweto na Jackson Matengula mkazi wa Uyole ambao ni baadhi ya waliojitokeza kupima afya zao walisema kuwa wanashindwa kupima afya zao hospitali kutokana na kutozwa fedha huku mapokezi yakiwa hayaridhishi.
Upimaji huo wa afya bure, unaishia kesho siku ya Mei mosi katika viwanja vya Sokoine kupitia mfuko huo wa taifa wa bima ya afya.